Ufaransa imefanikiwa kusonga mbele hatua ya robo fainali ya michuano ya kombe la Ulaya 2024 kupitia bao la kujifunga la dakika ya lala salama lililowapatia ushindi wa bao 1-0.

Juhudi za mshambuliaji wa Ufaransa Kolo Muani dakika ya 85 ya mchezo zilizaa matunda baada ya beki wa Ubelgiji Jan Vertonghen kujifunga na kuwapatia Ufaransa ushindi.


Kylian Mbappé kwa mara nyingine akiwa amevalia barakoa maalum ya kulinda pua yake iliyovunjika, alipata nafasi ya mikwaju takribani mitano lakini hakuna hata moja ambalo lilinasa nyavu za mlinda mlango Koen Casteels katika mechi baina ya miamba hiyo miwili ambayo inashikilia nafasi ya pili na ya tatu katika ubora wa soka duniani.

Kocha wa Ufaransa Didier Deschamps amekiri kwamba vijana wake wameshinda kwa taabu lakini ilikuwa mechi nzuri. " "Tulicheza mchezo mgumu dhidi ya timu kubwa, ingawa nadhani tulikuwa na mchezo wa kumiliki mpira zaidi na nafasi nyingi," alisema Deschamps.

MbappĂ© atakuwa akicheza robo fainali yake ya kwanza kabisa kwenye michuano ya Ulaya, huku Ufaransa ikiwa imepoteza kwa mikwaju ya penalti dhidi ya Uswizi katika hatua ya 16 bora kwenye michuano iliyopita mwaka 2021. 

Kati ya mabao matatu waliyofunga Ufaransa katika mechi nne za michuano hiyo, moja ni penalti ya Kylian Mbappe dhidi ya Poland huku mabao mengine mawili yakifungwa na mabeki wa timu pinzani.

Na katika mechi ya pili na ya kusisimua baina ya Ureno na Slovenia, mlinda mlango wa Ureno Diogo Costa anatajwa kuwa mchezaji wa mechi baada ya kuokoa mikwaju mitatu ya kwanza iliyopigwa na wachezaji wa Slovenia Josip Ilicic, Jure Balkovec na Benjamin Verbic.

Ureno imemaliza mechi hiyo kwa kuitandika Slovenia mabao 3-0 kwa njia ya mikwaju na kutinga hatua ya robo fainali. Mechi hiyo ilikwenda muda wa ziada baada ya dakika 90 kumalizika bila ya nyavu yoyote kufumaniwa.


Cristiano Ronaldo alitokwa na machozi baada ya kukosa penalti mnamo dakika ya 105 ya muda wa ziada na alionekana kufarijiwa na wachezaji wenzake kabla ya Benjamin Sesko wa Slovenia kukosa nafasi kubwa ya kuwaduwaza Ureno. Ronaldo pia alishindwa kutikisa nyavu kupitia mikwaju mitatu ya faulo huku matokeo yakisoma 0-0 baada ya dakika 120 kukamilika.

Machozi ya Ronaldo yaligeuka kuwa kicheko baada ya kupachika mkwaju wa penalti sambamba na mabao ya Bruno Fernandes na Bernardo Silva yaliyoisogeza Ureno hatua inayofuata na sasa itavaana na Ufaransa siku ya Ijumaa.

Slovenia inaondoka kwenye michuano hiyo ikiwa na sare nne baada ya kutoa upinzani mkali katika mechi yao ya kwanza kabisa ya mtoano.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement