Staa wa zamani wa Chelsea, Michy Batshuayi ameripotiwa kukumbana na meseji za vitisho vya maisha baada ya uhamisho wa Galatasaray.

Fowadi huyo mwenye umri wa miaka 30 mkataba wake utafika tamati mwishoni mwa msimu huu na anajiandaa kuachana na Fenerbahce.

Na sasa fowadi huyo wa kimataifa wa Ubelgiji, Batshuayi anajiandaa kwenda kujiunga na mahasimu wa timu hiyo, Galatasaray.

Hata hivyo, mkewe mrembo Amely Maria alituma meseji kwenye ukurasa wake wa Instagram akidai kwamba familia yao imekuwa ikiandamwa na meseji nyingi za vitisho baada ya kudaiwa mumewe ana mpango wa kwenda kujiunga na Galatasaray.

Mrembo Amely Maria aliandika hivi: “Wakati ambao hufahamu nini kitatokea kwenye giza, usimnyooshee kidole asiye na hatia. Watu wasiohitajika ni wale ambao hawataki kukubali majukumu yao.”

Amely aliongeza: “Aibu kwao wale wanaotishia maisha familia yangu, aibu kiasi gani!!! Wabaguzi na wenye kututisha, Mungu anawaona.”

Batshuayi alijiunga na Fenerbahce miaka miwili iliyopita na kufunga mabao 44 katika mechi 75.

Lakini, timu hiyo ilikuwa na msimu wa hovyo na hivyo kushindwa kubeba taji la Super Lig kwa tofauti ya pointi tatu.

Galatasaray iliipiku Fenerbahce kwenye kilele cha ligi hiyo na sasa wanataka saini ya Batshuayi.

Fowadi huyo wa zamani wa Crystal Palace anajiandaa kusaini mkataba wa miaka mitatu wenye thamani ya Pauni 50,000 kwa wiki.

Batshuayi alishazichezea timu nyingine za Uturuki ikiwamo Besiktas, ambako alifunga mabao 14 katika mechi 33 alipokuwa kwa mkopo akitokea Chelsea kabla ya kusaini Fenerbahce.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement