Kuanza jambo sio kazi bali kuliendeleza ndio mtihani unapoanza,Mafanikio ya jambo Fulani ni kutokana na jambo ambalo wewe mwenyewe ulilianzisha na likaonyesha mwanga wa wewe kukupa hayo mafanikio, Tanzania kwa sasa imekuwa nchi ya kutazamwa katika ukuwaji kwenye nyanja ya michezo.

Hongera kwenu TFF kwa kushirikiana na Serikali katika kuendelea kufanikisha hili, Kwa sasa kubwa lililopo kwenye vichwa vya watanzania wengi ni juu ya maandalizi ya Michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa maana ya AFCON 2027, sio jambo dogo, ni jambo kubwa sana nah ii inatokana na ukubwa wenyewe wa mashindano, Tanzania itashirikiana nanchi za Kenya na Uganda nah ii tunaiita ushirikiano utakaoleta manufaa kuanzia kwenye michezo na hata katika Sekta ya Utalii kwa nchi zote Tatu.

Hatujifunzi kwa walioshindwa bali tunajifunza kwa waliofanikiwa, mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni.

Sikwenda Ivory Coast lakini nilikuwa shuhuda wa karibu kuanzia maandalizi mpaka kuanza na kutamatika kwa mashindano hayo.

Walioshuhudia kwa asilimia kubwa mashindano hayo ni Shirikisho la Soka Barani Afrika kwa maana ya CAF, pongezi zikitolewa kutokana na maandalizi waliyoyafanya, Dk Patrice Motsepe Rais wa CAF alimuambia Rais wa FIFA Giani Infantino kuwa kwa kiwango cha maandalizi walichofanya Ivory Coast sasa ni wazi wanauwezo wa kuandaa Kombe la Dunia.

Hizi sifa zote hazijatoka hewani ila ni ukweli watu walifanya kazi kwelikweli.

Mashindano ya AFCON 2025 yanatarajiwa kufanyika Nchini Morocco , Taifa pekee la Afrika lililofanikiwa kufika Nusu Fainali Kombe la Dunia mwaka 2022.

Ufalme wa Morocco unauzoefu wa kuandaa mashindano na matukio makubwa kwa jumla hivyo kwao haya wanayamudu.

Ikumbukwe pia Morocco ilikuwa mtahiniwa wa kuandaa Kombe la Dunia 2026 japo alizidiwa kidogo na maombi ya Mrekani ya kaskazini, yaani Canada, mexico na Marekani.

Afrika Mashariki kupitia maombi ya pamoja ya Kenya, Tanzania na Uganda imepewa uenyeji wa AFCON2027.

Hii ni mara ya kwanza Afrika kwa Mataifa kuomba kuandaa mashindano kwa pamoja.

Sasa akili na mawazo ni katika miundombinu ya viwanja ambavyo ni muhimu sana kwa mashindano haya kwa jumla.

Serikali imethibitisha kuwa Michuano hiyo kwa upande wa Tanzania itachezwa Uwanja wa Benjamin Mkapa uliopo Dar es salaam, Uwanja wa Amaan uliopo Zanzibar na Uwanja mpya ambao utajengwa Jijini Arusha.

Uwanja wa Benjamin Mkapa unaendelea na marekebisho.

Uwanja wa Amaan ukiwa umekamilika, hii tunaita Indoor ya kwanza kwa Zanzibar na Alama iliyowekwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt: Hussein Mwinyi.

Rais Mwinyi ameweka alama nyingine ambayo itabaki katika kumbukumbu kwa Wazanzibar kwa kuwa na kiongozi wa kwanza wa visiwa hivyo kujenga Uwanja wa ndani kwa maana ya Indoor Visiwani humo.

Naamini Uwanja huo utakuwa bora sambamba na mingine miwili ya dar es salaam na Arusha kwa upande wa Tanzania katika maandalizi ya Michuano ya AFCON2027.

Uandaaji wa michuano hii kama nilivyosema itakuwa na Faida katika kukuza uchumi.

Katika Sekta ya utalii ambayo mbali na michezo inatajwa kwa jicho la kufungua Fursa zaidi na kuongeza watalii wapya katika sekta hiyo.

Kenya imewasilisha Uwanja wa Kimataifa wa Michezo wa Moi, Kasarani na Uwanja wa Taifa wa Nyayo.

Huku kwa upande wa mazoezi vikiainishwa kuwa vitatumika Viwanja vya Kasarani Annex, Police Sacco, Klabu ya Michezo ya Chuo cha Utalii Kenya, Ulinzi Sports Complex na Jamhuri Sports Complex.

Haya yote yasingewezekana, shukrani kwa wakuu wa nchi hizi tatu za jumuiya ya Afrika Mashariki, Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania, Yoweri Museven wa Uganda na William Ruto wa Kenya.

Hapa nina swali ambalo bado linaumiza kichwa, ni Mataifa ya Afrika Mashariki kuhakikisha wanaandaa timu zao za Taifa kuweza kufanya vizuri katika mashindano hayo.

Kwa kuwa wenyeji The Cranes, Harambee Stars na Taifa Stars hawatahangaika na hatua ya mtoano, lakini hata hivyo ukiondoa Uganda iliyowahi kufika Fainali miaka 46 iliyopita, Tanzania na Kenya wamekuwa wakiishia hatua ya makundi ya AFCON.

Hakuna jambo Baya kama mwenyeji wa mashindano kuondolewa mapema, Bila mwenyeji mashindanoni nguvu ya umma nyuma ya mafanikio ya mashindano haiwezi kupatikana, itakuwa ni sawa na kumuandalia mgeni karamu nzuri, ukamuacha mezani anakula halafu wewe ukaenda kuchungulia Dirishani anavyokula na kufurahia karamu uliyoiandaa wewe.

Serikali imetekeleza na imeendelea kutekeleza kwa upande wake na sasa ni wakati wa watu wa Ufundi kuchukua muda uliopo kufanikisha kwa upande wao. Tunasema Muda haupo upande wetu lakini kikubwa ni kupambana kuhakikisha tunafikia mafanikio.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement