Maafande wa JKU Wamemaliza ubishi kwa kutwaa taji la Ligi Kuu Zanzibar (ZPL), jana Ijumaa baada ya kutoka sare ya 1-1 na Kipanga, huku Zimamoto ikicharazwa mabao 2-0 na New City wakati ligi hiyo msimu wa 2023-2024 ikifikia tamati.

JKU na Zimamoto ndizo zilizokuwa zikichuana kuwania ubingwa huo uliokuwa wazi baada ya waliokuwa wakishikilia taji hilo, KMKM kulitema mapema.

Matokeo ya leo yaliyopatikana kwenye Uwanja wa Amaan B mjini Unguja, yameifanya JKU ifikishe pointi 66 na mabao 45 ya kufungwa na kufungwa 23, huku Kipanga ikimaliza nafasi ya saba ikiwa na pointi 40.

Kipigo cha Zimamoto ilichokutana nacho kwenye Uwanja wa Mao B kimeiacha timu hiyo ikisalia nafasi ya pili kwa kukusanya pointi 62.

Licha ya Kundemba kupata ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Malindi haikuizuia kushuka daraja ikizifuata Ngome, Jamhuri na Maendeleo iliyomaliza msimu kwa kulala mabao 4-2 na Hard Rock ikiweka rekodi ya kufungwa jumla ya mabao 73.

Kundemba imemaliza na pointi 35, lakini matokeo ya ushindi ya Hard Rock na New City yaliitibulia na kumaliza ya 13 na kukamilisha timu ya nne ya kushuka daraja kwa mujibu wa kanuni za ligi hiyo.

Bingwa huyo mpya wa ZPL atakabidhiwa Kombe Jumapili katika mechi maalumu itakayopigwa kwenye Uwanja wa New Amaan itakayoikitanisha JKU dhidi ya Bingwa wa Ligi Daraja la Kwanza Kanda ya Unguja, Muembe Makumbi.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement