Mahakama Kuu ya Tanzania Masjala ya Dar es Salaam inatarajia kusikiliza usuluhishi katika kesi ya kiungo nyota wa Yanga, Jonas Mkude ambaye anaidai Kampuni ya Mohamed Enterprises (Tanzania) Limited fidia ya Sh.1 Bilioni kwa kutumia picha yake katika matangazo ya biashara ya bidhaa zake bila ruhusa yake.

Kesi hiyo ya madai namba 192 ya mwaka 2023 ilikuja mbele ya Jaji Butamo Philip wa Mahakama hiyo leo Jumatatu, Novemba 20, 2023 kwa ajili ya kutajwa ambapo imepangwa kusikilizwa usuluhishi Novemba 27, 2023. Mbali ya kudai fidia hiyo Mkude ameiomba mahakama hiyo iamuru kampuni hiyo kumlipa mrabaha unaotokana na manufaa ambayo kampuni hiyo imeipata.

Katika madai hayo Mkude alilalamikia kampuni hiyo kutumia picha yake kutangaza biashara ya huduma zake na bidhaa kupitia mitandao ya kijamii ya Instagram Facebook na Twitter ikijulikana kama X bila ya kupata ridhaa kutoka kwake.

Mkude anadai Julai 12.2023 aliingia katika mkataba na kabu ya Yanga na akiwa na timu yake mpya anajiandaa na mechi alikutana na tangazo la biashara lenye picha yake likiwa katika mitandao hiyo ya kijamii.

Matangazo hayo yalisambazwa kupitia mitandao rasmi ya Twitter, Instagram na Facebook ya Mohamed Enterprises Limited (METL) ambayo aliweza kuyapiga picha (Screenshot) kuhifadhi na baadaye kuchapisha.

Anadai siku hiyo hiyo alianza kupokea simu nyingi na ujumbe mbalimbali kutoka kwa ndugu, jamaa, mashabiki na mwajiri wake wakimpongeza kwa kupata fursa hiyo ya matangazo huku wengine wakihitaji ufafanuzi juu ya suala hilo.

Katika hati hiyo inadai machapisho hayo yaliyopelekwa kwa umma yalipangwa kuandaliwa na kusambazwa bila ruhusa yake wala kuhusishwa kwa namna yeyote ili aweze kutoa idhini au kuruhusu kutumikia kwa picha ya kiungo huyo, Kwa kutumia picha ya Mkude kampuni hiyo ilipata umaarufu kwenye shughuli za kibiashara na kuvutia wateja ili watumie bidhaa zake kupata faida huku ikimyonya mdai huyo na kukiuka haki miliki.

Mkude alidai baada ya kutumiwa kwa picha zake bila idhini yake ameathirika kiuchumi na kisaikolojia ambavyo haviwezi kupata tiba pasipo kulipwa fidia hiyo ya Sh.1 bilioni kwa ukiukwaji huo bila idhini yake.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement