Yanga ipo kambini ikiendelea kunoa makali kwa ajili ya mechi za kimataifa dhidi ya CR Belouizdad ya Algeria na Al Ahly ya Misri, lakini benchi la ufundi chini ya Kocha Mkuu, Miguel Gamondi aliliitisha kikao na mastaa kwa ajili ya kujitathmini kwa mechi tisa za Ligi Kuu na nne za Ligi ya Mabingwa ili kujiweka sawa.

Kikao hicho kilichofanyika kwa muda wa dakika 45, kinaelezwa kilitumiwa na kocha kuwapiga mkwara mastaa hao ili kuhakikisha hawafanyi makosa kama yaliyowagharimu mbele ya Ihefu ambayo ni timu pekee iliyoifunga hadi sasa katika Ligi Kuu inayoiongoza na pointi 24 kutokana na michezo tisa iliyocheza.

baadhi ya mastaa wa Yanga waliohudhuria kikao hicho cha tathmini ya timu kwa vile wengine wameitwa kwenye timu za taifa za nchi zao zinazojiandaa na mechi za kimataifa za kuwani kufuzu fainali za Kombe la Dunia za 2026,

walikiri Gamondi na jopo lake wamesisitiza kupunguza rafu zisizo na ulazima huku wakikumbushwa kuhakikisha wanashambulia na kukaba kwa pamoja.

"Ijumaa muda mwingi tulitumia kuelekezwa vitu vya msingi kuelekea mchezo wa kimataifa tulisisitizwa sana kuhakikisha tunapunguza makosa yasiyo na ulazima na kufanya kazi kwa kushirikiana kama ni kushambulia tushambulie pamoja na kukaba ni jukumu letu sote," alisema Kennedy Musonda na kuongeza;

"Tumesisitizwa kadi nyingi za njano kimataifa zitatugharimu, hivyo tunapaswa kuwa makini kupunguza presha kwa benchi la ufundi." Beki Joyce Lomalisa alisema kikao hicho kilikuwa na lengo la kuwajenga na kupanga mipango yao kuhakikisha timu inafikia malengo na wanaendelea na mazoezi kama kawaida kujiweka fiti, ili kuendeleza rekodi Afrika.

"Tumeweka rekodi ya kutinga makundi baada ya miaka mingi iliyopita tuna kila sababu ya kufika mbali zaidi," alisema Lomalisa,

huku Kibwana Shomari akisisitiza huu ni msimu wa rekodi Jangwani malengo ni kutetea taji bila ya kupoteza mechi nyingi baada ya kuanza vyema msimu na kocha amekuwa akiwasisitiza kucheza kwa kushirikiana na kukaba kwa pamoja.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement