NYOTA wa Azam FC, Feisal Salum 'Fei Toto' amemfunika staa wa Yanga, Stephane Aziz KI kwa upachikaji wa mabao katika Ligi Kuu Bara.

Aziz KI aliyekuwa anaongoza kwa muda mrefu na mabao 10, amepitwa na Feisal ambaye amefikisha 11 msimu huu baada ya kufunga mawili wakati timu hiyo ya matajiri wa jiji la Dar es Salaam ikiibuka na ushindi wa 4-1, dhidi ya Dodoma Jiji.

Feisal alifunga mabao hayo dakika ya 62 na 64 huku mengine katika mchezo huo yakifungwa na Ayoub Lyanga na winga, Kipre Junior wakati lile la Dodoma Jiji likifungwa kwa mkwaju wa penalti dakika ya 84 na nyota wa timu hiyo, Emmanuel Martin.

Msimu huu umekuwa bora zaidi kwa Feisal tofauti na alivyokuwa Yanga kwa misimu miwili iliyopita kwani hajawahi kufikisha mabao zaidi ya saba.

Msimu wa 2021-2022 akiwa Yanga alicheza dakika 2044 katika michezo 26 kati ya 30 ya Ligi Kuu Bara ambapo alifunga mabao sita na kuchangia manne 'Assisti' huku msimu uliopita wa 2022-2023 akifunga pia sita tofauti na sasa alipofunga 11.

You Might Also Like

Get Newsletter

Advertisement